Mabaki ya wingu linaloendelea kupanuka tangu nyota GK Persei Farisi ilitazamiwa kuwaka kama nova mwaka 1902; picha ilipatikana kwa kuunganisha picha zilizopigwa katika upeo wa eksirei (buluu), nuru (njano) na wimbiredio (nyekundu);

Nyota nova (lat. stella nova kwa maana ya "nyota mpya", ing. nova) ni ongezeko la ghafla la mwangaza wa nyota. Ilhali idadi kubwa za nyota hazionekani kwa macho matupu ongezeko hili linatokea mara nyingi kama "nyota mpya" angani inayoweza kung'aa sana hata kushinda nyota zote nyingine. Hivyo inaonekana kwa muda tu na kupotea tena kwa mtazamaji asiye na darubini.

Historia ya utazamaji

Zamani nyota zote zilizowaka hivi ziliitwa kwa jina lilelile "nova". Jina hili lilitumiwa mara ya kwanza na Tycho Brahe ambaye katika mwaka 1572 aliona nyota mpya katika eneo la kundinyota Mke wa Kurusi (Cassiopeia) na kueleza utafiti wake katika kitabu cha "De stella nova"(Kuhusu nyota mpya) [1]. Wakati huo Tycho Brahe alianzisha majadiliano kuhusu mafundisho ya wataalamu wa kale walioamini kwamba hakuna mabadiliko yoyote kwenye anga ya nyota[2].

Hata kabla ya Tycho kulikuwa na taarifa kuhusu nyota zilizotokea angani. Taarifa ya kale zaidi ni ya wanaastronomia nchini China kwenye mwaka 185 baada ya Kristo kuhusu "nyota geni" iliyoonekana karibu na Rijili Kantori (α Centauri). Nova nyingine ilitazamiwa mwaka 1054 na kurekodiwa na wanaastronomia Wachina, Wajapani na Wakristo wa Baghdad. Mabaki yake huonekana hadi leo kama "Nebula ya Kaa" katika eneo la Tauri (Taurus).

Tofauti kati ya Nova na Supanova

Tangu karne ya 20 vipimo na elimu iliyopanuka vilifanya wanaastronomia kutofautisha kati ya "nova" na "supanova" ambazo zote ni "nyota mpya" zinazotokea angani kwa muda ila kwa sababu tofauti.

Tabia za nova

Nyota Kibete Cheupe inavuta mata kutoka Jitu Jekundu jirani kwake.

Nyota nova za kawaida zinatokea katika mfumo wa nyota maradufu. Nadharia inayokubalika na wengi inasema: nyota kibete cheupe na nyota kubwa, hasa jitu jekundu, zinazungukana kwa umbali wa karibu. Kibete cheupe kimeshamaliza hidrojeni yake na kujikaza, hivyo graviti yake bado ni kubwa ingawa mjao wake ni mdogo, pia ina joto. Jitu jekundu la jirani linaendelea kupanuka. Hapa sehemu ya mata ya tabaka za nje ya nyota kubwa inavutwa na graviti ya nyota ndogo na kuhamia upande wake. Sehemu ya mata hii ni hidrojeni inayokusanyika kwa umbo la diski ya uongezekaji[3] inayozunguka Kibete Cheupe na hatimaye kufikia karibu zaidi na kuunda angahewa. Hidrojeni hii inapashwa moto na uso wa Kibete Cheupe hadi kufikia halijoto ya kutosha ya kuanzisha myeyungano wa kinyuklia (nuclear fusion).

Mchakato huu unazalisha kiasi kikubwa cha nishati na kurusha sehemu ya hidrojeni inayowaka kwenye anga ya nje. Hii inaongeza mwangaza wa nyota inayoonekana sasa kama nyota nova. Kiasi cha masi inayorushwa angani wakati wa kuwaka inalingana takriban na 1/10,000 ya masi ya Jua.

Maendeleo ya nova inafuata hatua kama hizi:

Kugunduliwa kwa nova

Kila mwaka kuna takriban nyota nova 10 zinazotazamwa katika Njia Nyeupe[4]. Lakini wanaastronomia hukadiria kwamba idadi halisi ni kubwa zaidi, labda takribani 50 zinazotokea kila mwaka katika galaksi yetu[5].

Nyota nova zinagunduliwa pia katika galaksi nyingine, kwa mfano katika galaksi ya Andromeda (M31) na penginepo[6].

Nova za kurudia

Kinadharia mchakato huu unaweza kurudia mara kadhaa kwa sababu baada ya mlipuko wa angahewa ya nyota ndogo, mata kutoka jirani inaanza kuvutwa tena. Nyota RS Ophiuchi katika kundinyota ya Hawaa ilitazamwa kuwaka mara sita[7]: 1898, 1933, 1958, 1967, 1985 na 2006.

Hadi sasa kuna nyota nova 10 zilizotazamwa kuwaka tena kati ya takriban 400 zilizogunduliwa katika Njia Nyeupe[8]; kwa hiyo hakuna uhakika bado kuhusu muda wa kawaida uliopo baina ya kuwaka kwa nyota. Kama nyota kibete imeendelea kukusanya mata nyingi kuna uwezekano kwamba inalipuka mwishoni kama supanova [9]

Tanbihi

  1. Kilatini kwa "Kuhusu nyota mpya", linganisha Tycho's Supernova Remnant Archived 7 Agosti 2016 at the Wayback Machine., tovuti ya NASA, iliangaliwa Februari 2108
  2. Majadiliani yaliendelezwa na Johannes Kepler aliyeandika mwaka 1606 pia kuhusu "Stella Nova in pede Sagitarii" (kuhusu nyota mpya mguuni pa kundinyota Kausi)
  3. ing. "accretion disk"
  4. List of Novae in the Milky Way, tovuti ya Central Bureau for Astronomical Telegrams, iliangaliwa Februari 2018
  5. Shafter, A.W. (January 2017). "The Galactic Nova Rate Revisited". The Astrophysical Journal. 834 (2): 192–203
  6. M31 (Apparent) Novae Page, tovuti ya Central Bureau for Astronomical Telegrams, iliangaliwa Februari 2018
  7. Brandi, E.; Quiroga, C.; Mikołajewska, J. (2009). "Spectroscopic orbits and variations of RS Ophiuchi". Astronomy and Astrophysics. 497
  8. M. J. Darnley, V. A. R. M. Ribeiro1,2, M. F. Bode, R. A. Hounsell, and R. P. Williams, ON THE PROGENITORS OF GALACTIC NOVAE, The Astrophysical Journal, Volume 746, Number 1, Published 2012 January 25
  9. Sababu yake ni ya kwamba graviti yake inaweza kuzidi shinikizo ya mnururisho ndani yake ambayo kwa kawaida inatunza uwiano ndani ya nyota

Marejeo