Afande ni jina la heshima ambalo mwanajeshi au askari yeyote anamwita mkubwa wake. Inalingana na neno la Kiingereza "Sir" lililokuwa la kawaida katika jeshi wakati wa ukoloni wa Kiingereza.
Asili ya neno "afande" ni cheo cha effendi kilichokuwa cheo cha maafisa katika jeshi la Uturuki. Cheo hicho kilifika Afrika ya Mashariki kupitia askari Wasudani waliowahi kuhudumia katika jeshi la Misri katika karne ya 19; Misri ilikuwa sehemu rasmi ya Milki ya Osmani (ingawa ilijitegemea na kuwa chini ya athira ya Uingereza) ikatumia vyeo vya Kituruki katika jeshi lake.
Wajerumani walipoanzisha jeshi lao la kikoloni kwenye mwaka 1889 waliajiri askari Wasudani walioachishwa[1] kutoka jeshi la Misri na kuwapeleka Afrika ya Mashariki walipokandamiza upinzani wa Abushiri na watu wa pwani dhidi ya Wajerumani. Hao askari Wasudani waliendelea na vyeo walivyozoea, kama "shaush" kwa koplo na effendi kwa afisa. Effendi ilikuwa cheo cha afisa asiye Mzungu katika jeshi la Schutztruppe ya Afrika ya Mashariki[2]. Pia Waingereza walichukua askari Wasudani kwa ajili ya jeshi lao katika Kenya wakatumia "effendi" kwa ajili ya Waafrika waliopewa cheo cha afisa.