Nyotamkia ya Halley (jina rasmi 1P/Halley, kwa Kiingereza Halley's Comet) ni moja kati ya nyotamkia zinazozunguka Jua letu. Kila baada ya miaka 75 au 76 inapita karibu na Dunia ikionekana vema kwa macho matupu, hivyo ni mashuhuri. Itaonekana tena kwenye mwaka 2061.
Inazunguka Jua kwenye obiti yenye umbo la duaradufu. Wakati wa kuwa karibu na Jua (sehemu inayoitwa "periheli") inaonekana kwa muda wa wiki kadhaa kama nyota inayoota "mkia" yaani mstari mwangavu. Wakati inakwenda mbali na Jua mkia huo unapotea tena na kwa jumla haionekani tena kwa macho matupu ikikaribia "afeli" au sehemu ya mbali na Jua.
Jina limeteuliwa kwa heshima ya mwanaastronomia Mwingereza Edmund Halley aliyetambua ya kwamba nyotamkia aliyotazama mwaka 1705 ilikuwa ileile iliyowahi kutazamwa tayari katika miaka 1682(na Arnold), 1607 (na Johannes Kepler) na 1531 (na Petrus Apianus). Kwa hiyo alitabiri kurudi kwake mnamo 1758. Kweli ilionekana tena tarehe 25 Desemba 1758, miaka 16 baada ya kifo cha Halley. Katika mwaka uliofuata Mfaransa Nicolas Louis de Lacaille aliiorodhesha kama "comète de Halley".
Katika utaratibu wa Umoja wa Kimataifa wa Astronomia ilipokea jina la 1P/Halley. Namba 1 inataja nafasi yake ya kuwa nyotamkia ya kwanza iliyotambuliwa kisayansi, herufi P (ing. "periodic") inamaanisha ni nyotamkia inayorudi katika muda usiozidi miaka 200, Halley ni jina la mtambuzi. Nyotamkia zote zilizothibitishwa kuwa na obiti ya kurudia zimepokea namba pamoja na herufi P na jina la mtambuzi.
Wakati wa kupita karibu na Jua katika mwaka 1987 vipimaanga kadhaa vilirushwa juu na hasa kipimaanga Giotto kilifaulu kupata data nyingi. Halley ni gimba lenye umbo la kufanana na karanga. Urefu wake ni kilomita 15.3, unene kilomita 7.2. Uso unafunikwa na vumbi na rangi ni nyeusi.
Kutoka upande wa uso unaoangzwa na Jua kulikuwa na michirizi ya gesi na vumbi inayounda “mkia” wake. Upande huu kuna barafu iliyoanza kuyeyuka na kufoka nje. Gesi inayotoka ilipimwa kuwa maji 80%, monoksidi ya kaboni 10 %, methani na amonia 2.5% pamoja na viwango vidogo vya elementi nyingine kama feri na natiri.
Mwili wa nyotamkia ni mchanganyiko wa mawe, vumbi na barafu. Ikifuata obiti yake na kukaribia jua kiasi cha kutosha inaanza kuonekana kama nyota ikiakisi nuru ya jua. Ikikaribia jua zaidi sehemu ya barafu yake inaanza kuyeyuka kuwa mvuke unaotoka kwenye kiini cha nyotamkia yenyewe na kuizungusha kama angahewa. Gesi hii inasukumwa na upepo wa Jua (shinikizo ya miale ya nuru itokanayo na Jua) na kuonekana kama "mkia". Mkia huu unaelekea kila wakati upande usio wa jua kwa sababu upepo wa jua unasukuma mvuke upande ule.
Nyotamkia inaonekana kutoka Duniani wakati inakaribia periheli yake, yaani sehemu ya obiti ambayo ipo karibu zaidi na Jua. Tarehe ambazo Halley ilifika periheli zinaweza kukadiriwa kwa kutumia kanuni za fizikia. Taarifa ya kwanza iliyoweza kuthibishwa kuhusu nyotamkia ya Halley inapatikana katika kitabu cha historia ya China kuhusu kuonekana kwake kwenye mwaka 240 KK. Kwa jumla kumbukumbu ya wataalamu wa China inaonyesha taarifa nyingi katika karne za nyuma hadi kuboreka kwa astronomia na kumbukumbu yake katika magharibi yaani Ulaya na katika Mashariki ya Kati. Mipito mingine katika karne kabla ya Kristo iliripotiwa pia kwenye kumbukumbu ya Babeli.
25 Mei 240 KK (taarifa ya China) |
15 Machi 607 |
10 Juni 1456 |